Monday, December 3, 2012

Wakulima 40,000 Kiteto wabomolewa nyumba zao

WAKULIMA wapatao 40,000 waishio katika vijiji 11 vilivyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto, mkoani Manyara, hawana mahala pa kuishi baada ya nyumba zao kubomolewa na uongozi wa halmashauri hiyo.
Wakizungumza na waandishi wa habari kwa nyakati tofauti mwishoni mwa wiki wakazi hao ambao wanadaiwa kuvamia hifadhi ya mbuga ya Embloy Murtangosi, walisema wameonewa na kunyanyaswa kwa kuitwa wakimbizi kutokana na baadhi ya vigogo wa serikali kulitaka eneo hilo la hifadhi.Mmoja wa wakulima hao ambaye ni Mwenyekiti wa Kitongoji cha Leitimi, Majaliwa Mbaigwa, alisema wao ni wakazi wa wilaya ya Kiteto tangu mwaka 2003 na waliambiwa na halmashauri hiyo kusogea umbali wa kilomita mbili tu na si vinginevyo.
Alisema wamekuwa wakifanya shughuli zao za kilimo na kulipa ushuru wa halmashauri na kupatiwa risiti ikiwa ni pamoja na kuchangia shughuli za maendeleo kama ujenzi wa barabara, lakini cha kushangaza wanaitwa wakimbizi.
“Ajabu wameongeza eneo kutoka kilomita mbili hadi 20 na kutufanya sisi tuonekane tumevamia, jambo ambalo si halali,” alisema Mbaigwa.
Naye Anna Ngamia ambaye alikuwa akizungumza huku akilia, alisema kijiji cha Laitimi kipo toka mwaka 1985 bali ni hujuma ya wakubwa wenye hela ambao wanataka kuhodhi eneo hilo bila kujali utu na haki.
Kwa upande wake, Imamu wa Msikiti wa Laitimi, Hamisi Haji, alilaani bomoabomoa hiyo ambayo haikujali hata nyumba za ibada.