Wednesday, January 21, 2015

UFUGAJI WA SAMAKI

Ufugaji wa samaki kama ilivyo shughuli nyingine yoyote ya kiuchumi inahitaji usimamizi mzuri ili uweze kuwa na faida. Mbali na hilo, mfugaji wa samaki anatakiwa kuzingatia vigezo vingi kabla ya kuanza ufugaji. Moja ya vigezo hivyo ni soko. Si jambo la busara kuanza shughuli yoyote kabla haujafanya uchunguzi na kujua kama kuna mahitaji ya bidhaa unayokusudia kuzalisha. Wafugaji wengi wameanzisha ufugaji wa samaki lakini wakaishia kupata hasara kutokana na ukosefu wa soko. Na wengine wameanguka kutokana na utunzaji mbovu wa mabwawa ya samaki.

Maji
 Upatikanaji wa maji na ubora wake ni kigezo muhimu katika ufugaji wa samaki. Mtiririko wa maji ni njia rahisi kwa mfugaji. Maji machafu hayatakiwi kwa ufugaji wa samaki. Wafugaji ni lazima wasaidiwe na maafisa kilimo katika eneo lao kama maji yanayopatika yana ubora kwa ajili ya ufugaji wa samaki. Kwa wakazi wa Dar es
Salaam, inawezekana pia kufuga samaki kwenye bwawa, endapo maji yana chumvi ya wastani, na kwa kiwango kinachoshauriwa kitaalamu, basi samaki wanaweza kustahimili, na kukua vizuri.

Bwawa

Bwawa la samaki linahitaji nafasi kubwa ya ardhi, yenye mwinuko pamoja na eneo la samaki kukimbilia. Hii ni njia rahisi ya ufugaji endapo ardhi na maji havina gharama kubwa. Eneo kubwa zaidi linaruhusu uzalishaji usiohitaji nguvu ya ziada na wenye tija.

Utengenezaji wa bwawa la samaki kwa maeneo yenye udongo wa kichanga kama Dar es Salaam, mfugaji atalazimika kuchimba na kuweka karatasi ya nailoni. Hii, itasaidia kuzuia upotevu wa maji pamoja na kuzuia bwawa kuporomoka.

Ni vyema upande mmoja wa bwawa ukawa na kina kirefu kuliko mwingine. Upande mmoja unaweza kuwa na kina cha mita moja na nusu, na mwingine mita moja. Hii itamsaidia mfugaji kuweza kulihudumia bwawa vizuri, hata kama ni kuingia na kufanya usafi.

Utunzaji wa bwawa

Samaki 1Inashauriwa kufanyia bwawa usafi mara kwa mara, hasa kwa kuondoa majani ili kuepusha wadudu kufanya makazi na hatimaye wakawadhuru samaki. Pia ukiacha mimea bwawani itatumia virutubisho kwa kiasi kikubwa na kuondoa hewa ya oxijeni.
Hivyo, kila unapoona uchafu, safisha mara moja.

Ulishaji

Wafugaji walio wengi, wamekuwa hawazingatii kanuni za ulishaji wa samaki. Kwa kawaida inatakiwa kuwalisha samaki mara mbili hadi mara tatu kwa siku.

Aina ya chakula

Samaki wanaweza kulishwa kwa kutumia pumba ya mahindi, mashudu ya pamba na alizeti, soya, mabaki ya dagaa. Haishauriwi kulisha chakula kilichoko kwenye mfumo wa vumbi, bali kiwe mabonge madogo madogo, kwa wastani wa tambi.

Magonjwa

Kwa kawaida samaki hawana magonjwa mengi sana yanayowashambulia, ila kuna baadhi ya yaliyozoeleka kama vile magonjwa ya ukungu (fangasi), magonjwa yatokanayo na virusi, pamoja na minyoo.

Samaki wanaposhambuliwa na fangasi, huonekana kwa macho kwa kuwa huwa na madoa madoa. Samaki aina ya kambale hushambuliwa zaidi kuliko perege.

Pia unaweza kutambua kuwa samaki ni mgonjwa kwa kuwa huzubaa sehemu moja kwa muda mrefu. Magonjwa kwa samaki pia yanaweza kutokana na mrundikano kwenye bwawa. Hivyo, ni muhimu kuwapunguza kila wanapoongezeka.

Tiba

Tiba iliyozoeleka kwa samaki ni kwa kuweka chumvi kwenye maji, kasha kuwatumbukiza samaki unaowaona kuwa ni wagonjwa, kisha kuwatoa na
kuwarudisha bwawani.

Upatikanaji

Unaweza kupata vifaranga wa samaki kutoka katika kituo cha kuzalisha na kufuga samaki Kingolwira Morogoro. Bei ya kifaranga cha Perege ni shilingi 50, na Kambale ni shilingi 150.

1 comment:

  1. Nimeipenda hiyon Ngoja nijipange niingie kwenye hiyo biashara

    ReplyDelete