Tuesday, March 18, 2014

WANANCHI FUATILIENI MATUMIZI YA FEDHA ZA MIRADI'




MKURUGENZI Mtendaji wa Asasi isiyo ya kiserikali ya Pugu Poverty Alleviation and Development Agency (PPADA) Bw.Abraham Silumbu,amesema wananchi wamekuwa chanzo cha kuwepo kwa matumizi mabaya ya fedha kutoka kwa watendaji kutokana na kushindwa kufuatilia matumizi ya Fedha na Rasilimali za Umma (PETS) . 

Hayo yamebainika hivi karibuni wakati mkurugenzi huyo akizungumzia juu ya dhana ya misingi ya ufuatiliaji wa PETS katika kata mbalimbali nchini.
Alisema kuwa ili wananchi waweze kuwa na maendeleo ni wakati sasa wa kuhakikisha kuwa wanafuatilia fedha zinazotolewa na Serikali na si kukaa kimya kwani kwa kufanya hivyo ni kurudisha nyuma maendeleo. 

Alisema kuwa kuwepo kwa ufuatiliaji wa PETS kutaweza kusaidia kubaini ukweli na kuwasaidia kufanya maamuzi kwa kuwawajibisha watendaji wasio waadilifu na kuimarisha hali ya uwazi katika matumizi ya fedha na rasilimali zingine za umma. 

Alisema kuna kila sababu ya kuilaumu jamii kwa kutoshiriki katika ufuatiliaji wa matumizi ya fedha na rasilimali zao na kuchangia kuwepo na viashiria vya matumizi mabaya ya rasilimali zao.
Bw.Silumbu alisema Serikali imekuwa wazi kwa wananchi wake hasa kwa kutoa mwongozo elekezi wa jinsi ya kufanya ufuatiliaji huo, lakini wananchi wamekuwa kikwazo. 

Alisema kuwa mwongozo huo umetolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu -T
AMISEMI Desemba, 2009, ambao unawataka jamii wafanye ufuatiliaji wa matumizi ya fedha na rasilimali zao. 

Bw.Silumbu alisema jamii imekuwa ikilalamika juu ya kuwepo kwa matumizi mabaya ya rasilimali zao lakini hakuna jitihada zozote wanazofanya ili kuweza kupata haki hizo.
Alisema kuwa, asasi hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi chini wa Shirika la The Foundation for Civil Society (FCS) ambapo mpaka sasa tayari kata za Kitunda, Kivule, Msongola na Pugu zimefikiwa na mradi huu kwa awamu ya kwanza.

No comments:

Post a Comment