Wednesday, June 5, 2013

Wafugaji, wawindaji nchini waridhishwa Rasimu Katiba

Arusha
Mtandao wa Jamii za pembezoni za Wafugaji, Wawindaji wa Asili na Waokota Matunda, umeeleza kuridhishwa na rasimu ya Katiba Mpya iliyotambua uwapo wao na kulindwa rasilimali na tamaduni wao.
Mratibu wa Taasisi ya Katiba-Initiative iliyoundwa na mashirika yanayotetea jamii hizo, William Ole Nasha alisema mapendekezo yao mengi yamechukuliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
“Kimsingi tumeridhishwa na rasimu hii, maombi yetu mengi yameingizwa na sasa haki za jamii hizi, ambazo ni ndogondogo zitalindwa,” alisema Ole Nasha.
Pia, alisema haki za wafugaji ambao wamekuwa wakikabiliwa na matatizo mengi zimeingizwa na kwamba, sehemu nyingi ya rasimu itakuwa ikijulikana kuwa Tanzania kuna wakulima, wafugaji na wavuvi.
“Siyo kutambuliwa tu bali mifugo imetambuliwa kama zao la uchumi la wafugaji, pia ni maisha na mila,” alisema Ole Nasha.
Naye Mwanasheria wa Mtandao wa Mashirika ya Wafugaji wa Asili na Waokota Matunda (Pingo’s Forum), Emmanuel Saringe alisema wanaunga mkono rasimu hiyo, lakini walitaka wafugaji kuondolewa kwenye kundi dogo katika jamii.
“Wafugaji ni wengi hasa hawa wa asili, tungependa watajwe kama kundi kubwa ambalo linahitaji kutambulika ingawa kwa sasa linatajwa katika rasimu kama sehemu ya makundi madogomadogo,” alisema Saringe.
Alisema wafugaji ni kundi kubwa katika jamii, ambalo lipo nyuma kwa maendeleo, hivyo linapaswa kupewa kipaumbele na katiba.
“Wafugaji ni kundi maalumu, hivyo linapaswa kulindwa katika katiba na kuendelezwa kwani lipo nyuma,” alisema Saringe.

No comments:

Post a Comment