Wednesday, February 18, 2015

KNCU WAINGIZA MTAMBO MPYA WA KUKOBOLEA KAHAWA

Na Dixon Busagaga wa Globu ya Jamii kanda ya Kaskazini.

 CHAMA Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa zao la Kahawa mkoani Kilimanjaro KNCU (1984) Ltd kimetumia kiasi cha dola laki 9.48 kununua mtambo wa kukobolea Kahawa kutoka kampuni ya Pinhalense ya Brazil. 

 Ununuzi wa Mtambo huo wa kisasa unafanyika ikiwa ni sehemu ya maazimio ya mkutano mkuu wa KNCU uliofanyika mwishoni mwa mwaka jana wajumbe wakiazimia kufanyika juhudi za makusudi ili kukinusuru kiwanda hicho ambacho kilielekea kufa. 

 Katika hali ya kukiokoa kiwanda hicho,bodi ya kampuni ya kukoboa kahawa ya Tanganyika (TCCCo) ililazimika kuuza sehemu ya mali zake ili kukinusuru na madeni yanayokikabili baada ya kupata hasara ya zaidi ya shilingi bilioni 2 . 

 Tanzania Daima Jumatano ilifika katika kiwanda hicho juzi na kushuhudia sehemu za mtambo huo unaotajwa kuwa wa kwanza katika ukanda wa Afrika Mashariki na kati zikishushwa toka katika magari matano.

 Meneja wa TCCCO, Endrew Kleruu, alisema ujio wa mitambo hiyo utasaidia kupunguza upotefu wa Kahawa ,ikiwa ni pamoja na kuongeza ubora wa uzalishaji unaoendana na viwango vya ubora katika soko la Kimataifa. 

 Alisema mitambo hiyo yenye uwezo wa kuzalisha tani sita kwa saa moja itasaidia kuwapunguzia wakulima wa zao hilo gharama za uzalishaji kutokana na uwezo wake wa kutumia umeme mdogo wa Kilo Voti 30 hadi 35 tofauti na mtambo wa zamani ambao ulikuwa unazalisha tani nne tu kwa saa huku ukitumia zaidi ya Kilo Voti 100 ya umeme. 

 Kleruu aliwataka wakulima wa zao la Kahawa kuongeza juhudi katika kilimo cha zao hilo chenye tija ili kukidhi hitaji la Kahawa yenye ubora wakati wa uendeshaji wa mtambo huo mpya . 

 Kwa upande wake meneja wa usambazaji vifaa wa kampuni ya Brazafric Enterprizes Ltd, Salim Mghweno,alisema kuwa ufungaji wa mtambo huo utatumia miezi miwili ambapo matarajio ni hadi kufikia msimu wa uzalishaji wa Kahawa ufungaji wa mtambo huo utakuwa umekamilika. 

 Alisema kukamilika kwa ufungwaji wa mtambo huo kutasaidia ongezeko la kiwango cha zao hilo ukilinganisha na mtambo wa zamani ambao Kahawa iliyokobolewa ilipungua kiwango licha ya ukubwa wa mitambo ambayo pia imeelezwa kuwa ni chakavu. Mwisho.








Mtambo mpya wa kisasa wa kukobolea Kahawa ulionunuliwa na Chama Kikuu cha Ushirika cha Wakulima wa zao la Kahawa mkoani Kilimanjaro kwa gaharama za dola laki 9.48 ukishushwa katika kiwanda.
Mota ya kuzungusha mashine wakati wa ukoboaji ikishushwa ikiwa ni sehemu ya mtambo mpya wa kukobolea Kahawa utakaofungwa katika kiwanda cha Cofee Curing.
Sehemu ya vifaa kwa ajili ya mtambo mpya wa kisasa wa kukobolea Kahawa.

No comments:

Post a Comment