Thursday, May 16, 2013

Sh4 bilioni zatumika kwa kilimo Rukwa

Katika Kipindi cha mwaka wa fedha 2007/08 hadi 2010/11, Serikali imetoa Sh4 bilioni kwa ajili ya kusaidia miradi ya umwagiliaji katika Mkoa wa Rukwa , Bunge liliambiwa jana.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Naibu Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Adam Malima ambaye alisema kuwa fedha hizo zilipelekwa katika maeneo ya Sakalilo, Katuka, Singiwe, Maleza, Ulumi, Ng’ongo na Lwafi/ Katongo.
Malima alitoa kauli hiyo wakati akijibu swali la Abia Nyabakari (Viti Maalumu-CCM) ambaye alihoji ni kwa nini Serikali isione umuhimu wa kuupa kipaumbele Mkoa wa Rukwa katika masuala ya kilimo cha umwagiliaji.
Naibu Waziri alisema kuwa Serikali imekuwa ikiupa kipaumbele Mkoa wa Rukwa kutokana na ukweli kuwa unazalisha mazao mengi ya kutosheleza mkoa na kutoa ziada kwa mikoa mingine na ghala la Taifa.
Alisema katika kipindi hicho pia Serikali ilitoa ruzuku ya pembejeo za kilimo, mbolea na mbegu bora na kwamba jumla ya kaya 546,647 zilipata ruzuku hiyo hiyo pamoja na mbegu bora za mahindi bila matatizo.

No comments:

Post a Comment