Tuesday, May 7, 2013

Wakulima waaswa kuzingatia ushauri wa watafiti, watalaamu

WAKULIMA nchini wametakiwa kuzingatia ushauri wa watafiti na wataalam mbalimbali wa kilimo waweze kuzalisha mazao bora yenye tija katika soko la Afrika Mashariki (EAC).

Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Kilimo (IITA), Dk.Victor Manyong alisema endapo wakulima watazingatia ushauri watazalisha bidhaa bora zenye kukidhi matakwa ya walaji na hatimaye kuzalisha faida itakayowakwamua wao na familia zao.


Alisema IITA imekuwa ikifanya utafiti katika nchi mbalimbali za EAC kwa wakulima wadogo na kwa Tanzania tangu utafiti wa kilimo uanze mwaka 1994 kwa zao la mihogo na imeweza kuwaelekeza wakulima ni mbegu zipi zinafaa kulingana na ardhi yao.

“Kwa kushirikiana na Wizara ya Kilimo tumejikita katika utafiti mbalimbali na lengo kuu ni kuwasaidia wakulima waweze kulima kilimo cha kisasa kwa kutumia mbegu bora ambazo zitawasaidia kujiongezea kipato na kuachana na tabia ya kulima kwa mazoea,”alisema Manyong.

Alisema si kila mbegu au ardhi inafaa kwa kila zao hivyo kila fursa iliyopo inatumiwa kufanya utafiti na kugawa aina ya mazao yanayoonekana ni bora kwa majaribio kwa kuwapa wakulima ili na wao wajaribu na kutoa maoni yao.

Manyong alisema katika mkakati huo hadi sasa taasisi imeweza kubaini mbegu 18 za mihogo ambazo ni bora na zifaa kwa mkulima kupanda na kuzalisha faida kwa wingi endapo atazingatia maelekezo ya wataalam.

Alisema ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wakulima nchini taasisi imejenga jengo lenye maabara ya kisasa la utafiti ambalo linatarajiwa kulizinduliwa Mei 13 mwaka huu na Rais Jakaya Kikwete.

Manyong alisema kuzinduliwa kwa jengo hilo kutasaidia kuwapa uelewa zaidi wanafunzi na watalaam wa utafiti mbalimbali wa kilimo nchini.

No comments:

Post a Comment