Tuesday, February 25, 2014

MAHIZA AWAKUNA WAKULIMA WA KOROSHO



WAKULIMA wa zao la korosho mkoani Pwani wamefurahishwa na uamuzi wa Mkuu wa mkoa huo, Mwantumu Mahiza kutaka maofisa ushirika kuwajibishwa kwa kuwaondoa maofisa ushirika kutokana na utendaji mbovu na kushindwa kufuatilia madeni ya mikopo kwa vyama vya ushirika na fedha za wakulima wa zao la korosho. 

Mahiza alitoa agizo hilo kwenye kikao cha ushauri cha mkoa (RCC) kilichofanyika hivi karibuni mjini Kibaha na kubainisha kuwa ni kipindi kirefu aliomba matokeo ya kulipwa kwa madeni ya mikopo hiyo na fedha za wakulima hao suala ambalo usimamizi wake umeonekana sio wa kuridhisha.
Mkuu huyo wa mkoa alitaka kuwajibishwa kwa watendaji hao kutokana na vyama vya ushirika wa mazao (AMCOS) vilivyofanya biashara kwa kutumia mfumo wa stakabadhi za mazao ghalani msimu wa 2011/2012 kwa kutumia fedha kwa kukusanya mazao ya wakulima ambazo zilipatikana kutokana na mikopo toka kwenye taasisi za kibenki za NMB na CRDB ambapo jumla ya sh. bil 12 zilikopwa.
Mmoja wa wakulima wa zao hilo la korosho wilayani Kibaha, Peter Malundi alisema watendaji hao hawana msaada wowote hali ambayo inasababisha shughuli za kilimo cha zao hilo kutokuwa na manufaa kutokana na fedha zao nyingi kutolipwa kwa walikopwa korosho zao muda mrefu.
Malundi alisema kuwa hata deni hilo kubwa ambalo lilikopwa benki hizo kwa udhamini wa mkoa lingeweza kulipwa endapo watendaji hao wangekuwa makini lakini kutokana na kutowajibika ipasavyo kumechangia hali hiyo. 

"Kauli ya Mahiza kusema kuwa kwasasa hawataki watendaji hao ambao hawana manufaa na mkoa huo hususan wakulima hivyo haina budi kupitia kikao hicho kutamka rasmi hawafukuzi bali hawataki mkoani hapo kwa maslahi ya mkoa ni kauli inayoonyesha uwajibikaji na iwe fundisho kwa watendaji wengine," alisema Malundi.
Alisema kuwa baadhi ya watendaji ndani ya mkoa huo wamekuwa hawawajibiki na kuona kuwa Mkoa wa Pwani ni sehemu ya kupumzika pasipo kufanya kazi jambo hilo si sahihi kwani na wananchi wa mkoa huo nao wanataka maendeleo kama ilivyo mikoa mingine.
"Kwa kuwa mkuu wa mkoa alisema kuwa mwanzo wa mkakati wake wa mwaka 2014 kutaka uwajibikaji kwa watendaji kwenda kwa wananchi na kusimamia kero zilizopo pasipo kukaa kusubiri kero mezani kutoka kwa wananchi ni mpango mzuri," alisema Malundi.
Awali hatua iliyochukuliwa na Serikali kupitia wizara ya kilimo na ushirika iliwataka viongozi na watendaji wa vyama vya msingi kulipa madeni yaliyotokana na uzembe wao sambamba na kuwaondoa viongozi hao na kuteua bodi mpya.



No comments:

Post a Comment