Wednesday, February 26, 2014

USIMAMIZI HAFIFU WACHANGIA SAMAKI KUPOTEA MKOANI MARA


 

IMEELEZWA kuwa usimamizi hafifu wa kanuni na sheria za uvuvi ndani ya Ziwa Victoria ndio chanzo kinachochangia kupotea kwa samaki mkoani Mara. Kauli hiyo ilitolewa na Afisa Mfawidhi ulinzi na rasilimali za uvuvi Mkoa wa Mara, Braison Meela wakati akitoa taarifa katika kikao cha wadau wa uvuvi katika ziwa hilo kilichofanyika kwenye ukumbi wa uwekezaji uliopo katika Ofisi ya mkuu wa mkoa huo.

Meela alisema kuwa kumekuwepo na wasimamizi wabovu katika kusimamia kanuni na sheria ya uvuvi kuanzia ngazi ya kata hadi Taifa hali inayochangia kupungua kwa rasilimali hiyo ambayo ndiyo inayoingiza pato kubwa katika nchi hii .

Alisema kuwa lengo ni kuchukua hatua stahiki ili kuwa na rasilimali endelevu ya samaki katika ziwa hilo litakalofikiwa iwapo hatua sahihi na za makusudi zitachukuliwa dhidi ya wanaosababisha kupungua wingi wa samaki hao ndani ya ziwa.

Akizungumzia kuhusu changamoto zilizopo katika sekta hiyo alisema kuwa ongezeko la matumizi ya mbinu haramu ya uvuvi kama vile matumizi ya dawa za kilimo ya kuvulia samaki, usimamizi hafifu wa sheria na kanuni zake kama vile wataalam, BMU, wanasiasa na serikali ya vijiji ambapo matokeo yanaachwa yanaenda kama yalivyo ikiwa ni pamoja na ukosefu wa maadili na ukiukwaji wa miiko ya utumishi kwa baadhi ya watendaji.

"Nyavu za timba ni nyavu ambazo zimekuwa zikitumiwa mara kwa mara kuvulia samaki kwa njia ya uvuvi haramu na nyavu hizi zinatokea nchi za nje kwani wanaozingiiza ni wenzetu kwa kuwa wanajua bidhaa hiyo ina soko hapa kwetu hivyo tunapaswa kila mmoja kuwa mlinzi wa rasilimali hii," alisema Meela.

Akizungumzia viashiria vya kupungua kwa samaki alisema kuwa viwanda vya samaki vinazalisha kwa kiwango cha chini ya asilimia hamsini ya uwezo wake, hivyo kushindwa kukidhi mahitaji ya wateja wao.
Mmoja wa wadau hao ambaye ni mwenyekiti wa Halmashauri ya Butiama Magina Magesa alisema kuwa inashangaza sana kuona hapa nchini hakuna viwanda vinavyozalisha nyavu hizo, lakini nyavu hizo zimezagaa katika maeneo mbalimbali ndani ya nchi huku vyombo vya dola vimeshindwa kudhibiti uingizwaji wa nyavu hizo.

Mkuu wa Mkoa wa Mara John Tuppa akifungua kikao hicho alisema kuwa BMU ambao ndio kama ya kufuatilia matumizi mabaya ya zana hizo lakini hao ndio wanaowakingia kifua wavuvi haramu kwa kuwaambia wafiche zana hizo wakati wa oparesheni ili wakimaliza waendelee na shughuli zao kama kawaida.

Alisema nchi jirani zinazozungukwa na ziwa hilo wananufaika na mazao ya ziwa hilo lakini Mkoa wa Mara umeshindwa kunufaika na mazao yanayotokana na ziwa hilo kwa sababu ya watu wa BMU kutokuwa na maadili ya utendaji kazi kama dhamana yao.


 


No comments:

Post a Comment