Tuesday, February 25, 2014

WAKULIMA WA PAMBA WAMLALAMIKIA RC




CHAMA cha Wakulima wa Pamba nchini (TACOGA) kimemlalamikia Mkuu wa Mkoa wa Geita, Magalula Said Magalula, kwa kitendo chake cha kuagiza kukamatwa na kuwekwa ndani kwa wawekezaji watatu wa zao la pamba akiwatuhumu kushindwa kufunga mikataba na wakulima .
Kwa mujibu wa tamko lililotolewa kwa waandishi wa habari juzi mjini Kahama mkoani Shinyanga na mwenyekiti wa TACOGA, Elias Zizi, kitendo cha hicho kinadaiwa kupingana na agizo lililotolewa hivi karibuni na Rais Jakaya Kikwete, alipoagiza wakulima wasilazimishwe kujiunga na mpango wa kilimo cha mkataba mpaka pale watakapokuwa wamepewa elimu ya kutosha.

Zizi aliwataja wawekezaji waliokamatwa na kuwekwa ndani kwa agizo la mkuu huyo wa mkoa kuwa ni pamoja na mwakilishi wa kampuni ya Fresho Investment, Kampuni ya ICK Cotton Co. Ltd na Kahama Oil Mill Ltd ambao wote wanafanya shughuli zao katika mkoa huo wa Geita.

Mwenyekiti huyo ameelezea kushangazwa kwake na hatua ya mkuu wa mkoa huo ambayo amedai ni matumizi mabaya ya madaraka aliyopewa na Rais Kikwete na kwamba mpango wa kilimo cha mkataba pamoja na kuwa ni hiari hata hivyo baada ya majaribio yake kulijitokeza changamoto kadhaa katika utekelezaji wake.

Akifafanua, alisema baada ya kujitokeza kwa changamoto hizo wadau wote walikubaliana kusitishwa kwa muda utekelezwaji wa mpango huo mpaka pale changamoto zilizojitokeza zitakapopatiwa utatuzi ikiwemo suala la elimu duni juu ya mpango huo kutobainishwa vizuri kuhusu faida au hasara zake.
Kutooneshwa wazi kwa bei ya pamba atakayolipwa mkulima pale atakapokuwa anauza pamba yake licha ya kukopeshwa huduma zote muhimu ambazo bei zake zinafahamika pamoja na kilimo hicho kutokuwa na bima itakayomlinda mkulima iwapo patatokea janga lolote kama vile suala la ukame.
"Lakini changamoto nyingine ni suala la vikundi vya wakulima kutosajiliwa kisheria hali inayowanyima haki ya kudai na kudaiwa kisheria, uwekezaji mdogo wa mkopeshaji ukilinganisha na jasho la mkulima wa pamba analowekeza kwa eneo moja.
"Sisi TACOGA tunalaani kitendo cha Mkuu wa Mkoa wa Geita kwa hatua ya kutoa agizo la kukamatwa kwa wawekezaji hao katika zao la pamba ambapo wanatoa huduma katika mkoa wake, kitendo hicho kimelenga kuzishinikiza pande mbili pasipo hiari yao kuingia kwenye kilimo hicho cha mkataba."
Naye Mkuu wa Mkoa wa Geita, Magalula, pamoja na kukiri kutoa agizo la kukamatwa na kuwekwa ndani kwa wawekezaji hao alikanusha sababu zilizotolewa na viongozi wa TACOGA na kufafanua kuwa kosa lao ni lakuwauzia wakulima viuatilifu kwa fedha taslimu badala ya kuwapa kwa mkopo kama yalivyo maelekezo ya Bodi ya pamba (TCB).
"Nikweli nilitoa agizo wakamatwe, lakini hao TACOGA wanapotosha ukweli, sijawakamata kwa kutokuwa na vikundi vya kilimo cha mkataba, bali ni kutokana na kukiuka kwao utaratibu wa usambazaji dawa hizo za kuua wadudu ambapo mbali ya kuuza kwa fedha taslimu fedha hizo hawakuziwasilisha bodi ya pamba ambayo ndiyo iliyowapatia dawa hizo," alieleza Magalula.



No comments:

Post a Comment