Tuesday, March 11, 2014

NMB YASIFIWA KWA KUKOPESHA WAJASIRIAMALI




NMB imepongezwa kwa kuwa benki ya mfano kwa kuwawezesha wajasiriamali, kukopa pikipiki kwa kuchangia asilimia 30 kama malipo ya awali, kiasi ambacho Watanzania wengi wanaweza.

Pongezi hizo zimetolewa jana na Waziri wa Nchi katika Ofisi ya Waziri Mkuu(Uwekezaji na Uwezeshaji), Dk Mary Nagu wakati akizindua mradi wa ukopeshaji wa bajaj na pikipiki, unaotolewa na benki ya NMB.

Dk Nagu alitoa mwito kwa benki na taasisi za fedha nchini, kubadili fikra na mtazamo wa utoaji wa mikopo, ambao utawawezesha Watanzania wengi zaidi kukopa na kufanya biashara.

Alisema utaratibu wa kung’ang’ania dhamana ya mali zisizohamishika katika utoaji wa mikopo, umepitwa na wakati.

“Taasisi za fedha nchini inabidi zibuni njia mbadala kama ilivyofanya NMB za kutoa mikopo kwa wananchi wengi zaidi bila kutumia dhamana ya mali zisizohamishika na endapo watafanya hivyo watakuwa wanajenga uwezo wa wananchi kuweka amana kwenye benki zao,” alisema.

Alisema changamoto kubwa inayowakabili wajasiriamali nchini ni ukosefu wa mitaji, masharti magumu ya benki na riba kubwa. Hata hivyo, Dk Nagu aliwashauri wakopaji wa vyombo hivyo vya usafiri, kukatia bima ili tatizo likitokea wasirudi nyuma zaidi kiuchumi kwani watatakiwa kuendelea kurejesha mikopo.

Aidha, alitoa rai kwa madereva wa bodaboda, ambao wengi wao ni vijana, kuzingatia sheria za usalama barabarani ili wasipunguze mapato yao kwa tozo mbalimbali, wanapovunja sheria.

Kwa upande wake, Mkuu wa Kitengo cha Biashara za kibenki wa NMB, Filbert Mponzi alisema mikopo hiyo imebuniwa baada ya kuona changamoto kubwa ya ajira kwa vijana hapa nchini.

Alisema mikopo hiyo ilianzishwa mwaka jana mkoani Dar es Salaam na baada ya kuona inakubalika wameongeza kasi ya kuipeleka mikoa mingine.

Alisema marejesho hufanyika katika kipindi cha miezi 24 na kwamba ili kumlinda mteja, mikopo hiyo imewekewa bima kwa ajili ya ulemavu na kifo kitakachomtokea mmiliki wa pikipiki iliyochukuliwa mkopo.



No comments:

Post a Comment