Friday, March 14, 2014

WAJASIRIAMALI WAUNGANA ILI KUTUNISHA MFUKO





WAJASIRIAMALI waliopo kwenye vikundi saba tofauti vya Kuweka na Kukopa ndani ya Kijiji cha Kidogozero Wilaya ya Bagamoyo Mkoa wa Pwani wameungana na kuwa na kikundi kimoja chenye nguvu kiitwacho Tukishirikiana Tunaweza.

 Akizungumza mbele ya wanavikundi hao pamoja na maofisa kutoka Plan International Bi.Jema Helman na Bw.Kulwa Daud wa UHIKI, Mwenyekiti wa kijiji cha Kidogozero, Ally Mmanga alisema kuwa hatua hiyo inalengo la kupata kikundi kimoja chenye nguvu ambacho kitakuwa na uwezo wa kupata mikopo kutoka kwa mashirika mbalimbali ili kujiinua zaidi kiuchumi.

Mmanga amevitaja vikundi ambavyo vimeungana kuwa ni Vijana Jembe, Wanawake Tunaweza, Juhudi, Jitihada, Mshikamano, Jikomboe na Maskini Tunaweza umoja ambao unajumuisha wanachama wapatao 218.
"Sisi viongozi waserikali kwanza tulikaa na viongozi wa vikundi hivi saba na kuwafikishia mawazo yetu ya kuwataka waungane kwa lengo la kupata kikundi kimoja chenye nguvu, tunashukuru wazo letu wakalikubali walipokwenda kuzungumza na wenzao wakafikia maamuzi na hii leo tutapata viongozi wa muda ambao watauongoza umoja huo," alisema Mmanga. 

Alisema kwamba lengo pia ni kutunisha mfuko wa muungano wao ili waweze kukopeshana kwa masharti nafuu, kupata pembejeo pamoja na zana za kilimo kama trekta ili kurahisisha kilimo kwa wajasiriamali hao.
Kwa upande wake Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, Bi. Zakia Digoo alisema kuwa hatua hiyo inaunga mkono juhudi za serikali ambayo inawataka wananchi kujiunga kwenye vikundi kwa lengo la kuwafikia kwa urahisi zaidi kupitia mikopo mbalimbali. 

Kwa upande wao maofisa hao kutoka Plan na UHIKU wamewataka viongozi hao kuhakikisha wanawasiliana na ofisi hizo kwa ushauri ili malengo yao yaweze kuwa na mafanikio na kwamba watakuwa karibu nao kufanikisha malengo yaliyowekwa na umoja huo. 

Baada ya mkutano huo wana-umoja hao waliteua viongozi ambao watawaongoza katika kipindi hiki ambapo Mwenyekiti ni Said Sango, Ramadhani Kibambe Katibu huku Mhazini akiteuliwa Nuru Lichapwike.
Akitoa shukrani kwa niaba ya umoja huo mwanachama Shaha Kiwilima alianza kwa kutoa shukrani kwa serikali ya kijiji pamoja na wataalamu hao na kueleza kwamba watajipanga kikamilifu ili kuona malengo yao yanakuwa na mafanikio.


No comments:

Post a Comment