Monday, March 10, 2014

WASAJILI WA KAMPUNI WATAKIWA KUWA MAKINI




WADAU wanaoshughulika moja kwa moja na mchakato wa usajili wa kampuni hapa nchini, wametakiwa kufanya kazi kwa karibu zaidi ili kuimarisha kiwango cha Tanzania kimataifa katika kujenga mazingira ya biashara.

Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Dk Florens Turuka amesema hayo jana jijini Dar es Salaam wakati wa mkutano wa CEO Roundtable.

Alifafanua kuwa mamlaka hizo zinatakiwa kutekeleza mradi unaojulikana kama Tanzania Investment Window Project kabla ya Mei mwaka huu ili faida za ubunifu wake uunganishwe katika viwango vya mwaka kesho vinavyohusu jinsi nchi zinavyoimarisha mazingira ya biashara.

Mradi huo unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo (UNDP) na mpango wa ONE UN, unalenga kuwezesha kampuni za ndani na za nje kujisajili kwa urahisi zaidi na kwa muda mfupi.

Kituo cha Uwekezaji nchini (TIC) kwa msaada wa kiufundi kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa Linalohusika na Biashara na Maendeleo (UNCTAD) liko katika juhudi kuhakikisha kuwa taratibu za usajili wa kampuni unarahisishwa kupitia mtandao.

Mpango huo uliasisiwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda mwezi Oktoba mwaka jana nchini China.

Mpango huo utaruhusu wawekezaji kusajili kampuni, kupata vibali vya uwekezaji, vibali vya kazi na huduma nyingine kupitia njia ya mtandao.

Dk Turuka alitaja baadhi ya taasisi zinazotakiwa kufanya kazi kwa karibu kama Wakala wa Usajili wa Makampuni (Brela), Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Wizara ya Biashara, Mamlaka ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), Jiji la Dar es Salaam na TIC.

No comments:

Post a Comment