Friday, March 7, 2014

KENYA KUANZISHA ENEO LA KWANZA LA BIASHARA HURIA




Serikali ya Kenya tarehe 13 ilifanya mkutano wa baraza la mawaziri ikiidhinisha kuanzisha eneo la kwanza la biashara huria mjini Mombasa. 

Mkutano huo ulioongozwa na rais Uhuru Kenyatta. Sababu ya kuidhinisha kuanzisha eneo la biashara huria ni kwamba serikali ya Kenya imetambua kuwa uchumi wa dunia unafufuka, na uchumi wa nchi za Afrika zilizoko kusini mwa jangwa la Sahara una mwelekeo mzuri, na mambo hayo yote yameonesha mustakabali mzuri wa uchumi wa Kenya. 

Mji wa Mombasa ni mji wa pili kwa ukubwa nchini Kenya, ni bandari kubwa zaidi nchini humo, pia ni kituo muhimu cha viwanda na biashara. Mji huo umeunganishwa na mji mkuu Nairobi kwa reli, barabara kuu na mabomba ya kusafirisha mafuta. Bandari ya Mombasa ina vifaa vya kisasa, ambayo inashughulikia uchukuzi wa baadhi ya bidhaa za Kenya, Uganda, Tanzania, Burundi na Rwanda. Bandari hii iko katikati ya pwani ya Afrika Mashariki. Hakuna bandari kubwa kaskazini yake hadi bahari nyekundu, na kusini yake kuna bandari ya Durban ya Afrika Kusini tu ambayo ina uwezo wa kushindana na bandari hii. Sababu zote hizi zimeweka mazingira mazuri ya kuanzisha eneo la kwanza la biashara huria mjini Mombasa. 

Licha ya Mombasa, serikali ya Kenya pia inapanga kuanzisha maeneo ya biashara huria katika miji ya Kisumu na Lamu. Hivi sasa imetenga ardhi kilomita 3,400 za mraba kwa ajili ya ujenzi wa maeneo ya biashara huria. Eneo la biashara huria la Mombasa litakuwa kilomita elfu 2000 za mraba, lile la Kisumu na lile la Lamu yote ni kilomita 700 za mraba. 

Taarifa zilizotolewa na serikali ya Kenya zinaonesha kuwa, ushuru wa bidhaa utafutwa katika maeneo hayo ya biashara huria, na hatua hii itaimarisha na kuboresha biashara kati ya nchi za Afrika Mashariki, ya Kati na Kusini. Pia Kenya inatazamiwa kuagiza bidhaa za nchi hizi moja kwa moja katika maeneo ya biashara huria badala ya kwenda Umoja wa Falme za Kiarabu, China na Japan.

WANAVIJIJI WENGI ZAIDI WA CHINA WAANZA KUFANYA BIASHARA KUPITIA INTERNET




Bibi Li Haibo ni ofisa wa kamati ya kijiji kimoja kilichoko kaskazini mashariki mwa China. Mwezi huu amepata kazi mpya, ambayo ni kuwafundisha na kuwaelekeza wanakijiji kufanya biashara kupitia Internet, ili kuwasaidia kuongeza kipato chao.

Mwishoni mwa mwezi Februari, mkoa wa Jilin ulifanya mkutano wa mafunzo ya wafanyabiashara kupitia Internet. Viongozi wa idara za biashara za kaunti mbalimbali na wahitimu wa vyuo vikuu wanaofanya kazi katika kamati za vijiji mkoani humo, walikusanyika pamoja kusikiliza mafunzo ya wataalamu wa kampuni ya Alibaba ambayo ni kampuni maarufu inayotoa huduma ya biashara kupitia Internet nchini China.

Mkoa wa Jinlin ambao unazalisha mazao ya kilimo kwa wingi lakini uchumi hake haujaendelezwa vizuri, ulipanga kuwasaidia wakulima katika vijiji 100 kufanya biashara ya bidhaa zenye sifa ya kipekee za huko kupitia Internet.

Takwimu zilizotolewa na kituo cha utafiti cha Ali kinachomilikiwa na kampuni ya Alibaba zinaonesha kuwa, hadi tarehe 30 Novemba mwaka 2013, maduka ya ngazi ya vijiji na miji midogo yaliyosajiliwa kwenye tovuti ya Taobao.com yalikuwa milioni 1.05. Idadi hiyo iliongezeka kwa laki 4 na 60 elfu kuliko mwaka 2012, ambalo ni ongezeko la asilimia 76.3.



Bibi Li Haibo sasa ni naibu katibu wa kamati ya chama ya kijiji cha Erdaohezi mjini Dunhua mkoani Jilin. Ni mhitimu wa chuo kimoja cha uchumi, na alianza kufikiria njia ya kuwasaidia wanakijiji kuuza mazao ya ginseng na uyoga mweusi.

Bibi Li anasema, hata katika vijiji viliyoko nyuma kiuchumi, watu wananunua bidhaa kwa wingi kupitia Internet, na makampuni mbalimbali ya usambazaji wa vitu yameanzisha matawi yao vijijini, hivyo biashara kupitia Internet ina mustakabali mzuri.

Gongzhuling ni moja ya kaunti zilizoko mkoani Jilin. Mamia ya makampuni ya huko yameanza kuuza bidhaa zao kupitia Internet, lakini bidhaa nyingi zinauzwa katika kaunti hii tu.
Mkurugenzi wa idara ya biashara Bw. Sun Dianpu ana mpango wa kuwaelekeza wazalishaji na wauzaji kujifunza ujuzi kuhusu biashara kupitia Internet, kuanzisha maduka kwenye tovuti, na kuuza mahindi na maharagwe yanayozalishwa huko nchini kote.

Katika mikoa ya pwani ya Jiangsu, Zhejiang na Shandong, baadhi ya vijiji vimepewa jina la "vijiji vya Taobao", kwa sababu maelfu ya wanavijiji wameanzisha maduka yao kwenye tovuti ya Taobao.com.

Ripoti ya maendeleo ya biashara kupitia Internet katika kaunti za China mwaka 2013 iliyotolewa na kituo cha utafiti cha Ali mwezi Januari inaonyesha kuwa, kati ya kaunti 100 zinazopata maendeleo zaidi katika biashara kupitia Internet, kauti 49 ni za mkoa wa Zhejiang.

Katika kijiji cha Liucun mjini Yiwu mkoani Zhejiang, karibu kila familia inashughulikia mauzo ya bidhaa kupitia Internet. Thamani ya mauzo ya maduka zaidi ya 2000 ya wanakijiji hao ilikuwa yuan bilioni 2 mwaka jana.

Mkoa wa Jilin pia umechukua hatua ya kujenga "vijiji vya Taobao" na kaunti za biashara kupitia Internet. Jumba la Jilin ni moja kati ya jukwaa kubwa la biashara linalojengwa.

Mkurugenzi wa idara ya biashara ya Jilin Bibi Cong Hongxia anasema, jumba hilo litakusanya bidhaa kutoka sehemu mbalimbali, zikiwemo mchele, maharagwe, ginseng, vyura, maji yenye madini, uyoga mweusi na matunda ya blueberry yanayozalishwa kwenye mlima Changbai.

Naibu meneja mkuu wa kampuni ya Alibaba Bw. Gao Hongbing anasema, mikoa ya pwani iliyoko kusini mashariki mwa China imetangulia kuendeleza biashara kupitia Internet na imepata maendeleo ya kasi. Ingawa mikoa iliyoko kaskazini mashariki na kaskazini magharibi mwa China ilichelewa kuendeleza shughuli hizi, lakini bado inaweza kupata fursa nyingi.

Takwimu za kituo cha utafiti cha Ali zinaonesha kuwa, hadi mwezi Desemba mwaka jana, China imekuwa na "vijiji 20 vya Taobao", ambavyo viko katika mikoa saba ikiwemo Hebei, Shandong, Jiangsu, Zhejiang na Guangdong. Wanavijiji wa vijiji hivyo wameanzisha maduka elfu 15 kwenye tovuti ya Taobao.com ambayo yanashughulikia mauzo ya bidhaa za majumbani, nguo, mifuko, mazao ya kilimo, bidhaa ndogondogo, na vitu vinavyotumiwa wakati wa michezo au utalii. Shughuli hizi zimewasaidia wanakijiji elfu 60 kupata kazi.

Kituo cha utafiti cha Ali kinasema, kama zaidi ya asilimia 10 ya watu katika kijiji kimoja wanafanya biashara kupitia Internet, na thamani ya mauzo inazidi yuan bilioni 10, basi kijiji hicho kinaweza kuitwa "kijiji cha Taobao".

Wataalamu wanaona kuwa, wanavijiji wengi kufanya biashara kupitia internet ni jambo la kipekee nchini China, na mwaka huu biashara hiyo itaendelea kupata maendeleo ya kasi.

BENKI YA AFRICA KUTOA MIKOPO KWA WAFANYABIASHARA WADOGO NCHINI




Benki ya Africa (Boa) imesaini mkataba wa Sh. bilioni 15 na European Investment Bank kwa ajili ya kutoa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo na wakati nchini ili kuinua biashara zao.

Mkataba huo ulisainiwa juzi jijini Dar es Salaam na viongozi wa Boa Tanzania na Balozi wa European Investment Bank, Filberto Ceriani, sasa wafanyabiashara sasa ni wakati wao kwenda BOA benki kwaajili ya kujipatia mkopo wako katika kuongeza ufanisi wa biashara yako.

Wakizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam juzi, Afisa Mwandamizi wa European Investment Bank, Pim Van Ballekom na  Mkurugenzi wa Boa, Ammish Owusu Amoah walisema zimetolewa Euro milioni saba  sawa na Sh, bilioni 15 kwa ajili ya kutoa mikopo kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati wa hapa nchini.

Walisema wameamua kufanya hivyo ili kutoa nafasi kwa wafabiashara wadogo na wakati kuendeleza biashara zao na hivyo kujikwamua kimaisha, pia walisema  kuwa, mikopo hiyo itatolewa kwa kuzingatia kigezo cha biashara ya mtu anayeomba na wanaanzia Sh. milioni 25 ambazo zinatakiwa kurudishwa kwa wakati muafaka ambao umepangwa na benki hiyo.

Walisema benki ya Boa ilianza muda mrefu kutoa mikopo hiyo na na kwamba fedha hizo kutoka European Bank ni nyongeza na kuahidi watatoa mikopo hiyo ili wafanyabiashara wanufaike nayo katika biashara zao.

Amoah alisema wamefurahi kuona European Bank wanatambua mchango wao na kuamua kuwaongeza fedha za kusaidia wajasiriamali wadogo na wa kati ambao wengi wao wanafanya biashara bila ya kujua mikopo yao wanaipata wapi.

Alisema vigezo vitakavyotumika kwa ajili ya kutoa mikopo hiyo ni pamoja na muombaji kuonyesha biashara yake ambayo itakaguliwa ili uweze kupatiwa mkopo kwa ajili ya kuiendeleza. - See more at: http://ajirazetu.com/blog/227-benki-ya-africa-kutoa-mikopo-kwa-wafanyabiashara-wadogo-nchini.

WAFUGAJI WA TARIME WATAKA VIWANDA VYA MAZAO YA MIFUGO





Tarime. Wafugaji katika Kijiji cha Matongo-Nyamongo wilayani hapa wameiomba Serikali kufufua viwanda vya maziwa, ngozi na kuanzisha viwanda vya kusindika nyama ili kumkomboa mfugaji kimaendeleo kwa madai kuwa kukosekana kwa viwanda hivyo kunapelekea mifugo kuuzwa Kenya.

Wafugaji hao walisema, kuwapo kwa viwanda hivyo mkoani Mara kumesaidia kupata uhakika wa soko la bidhaa zao zinazotokana na mifugo na hivyo kupata faida na maisha yao kusonga mbele kwa kuwa watapata pesa na kujiletea maendeleo.

Wakiongea na gazeti hili kwa nyakati tofauti, wafugaji hao walisema kuwa, licha ya kumiliki mifugo mingi lakini hawaoni manufaa yake kwani kwa sasa lita moja ya maziwa wanauza kwa Sh1000 kutoka kwa mnunuzi mmoja mmoja pindi anapohitaji.



Lazack Kesongo mmoja wa wafugaji hao wa ng’ombe,alisema mifugo waliyonayo haiwasaidii katika kutatua matatizo yao ya kifamilia na kwamba kuisihi Serikali kuliangalia kwa umakini ombi hilo la kujengwa kiwanda cha ngozi.

Mkuu wa Wilaya ya Tarime, John Henjewele ameunga maoni hayo ya wafugaji na kusema kuwa kuna haja kweli ya Serikali na wawekezaji kufufua viwanda vya maziwa hususani mkoani Mara kwa madai kuwa kuna viwanda vingi vya maziwa ambavyo havifanyi kazi kutokana na kukosa watu wa kuzalisha.

Henjewele alisema, kutokuwapo kwa viwanda Tarime vya maziwa, ngozi na kusindika nyama, wafugaji wamekosa maendeleo na kwa sababu hiyo wafugaji hao huuza mifugo yao Kenya kwa kuwa huko kuna viwanda.

Kaimu Ofisa Mifugo, Juma Mganga alisema kuwa halmashauri ina mpango wa kuanzisha vituo vidogo vya kuuzia maziwa ambapo watu watapeleka kuuza maziwa yao na mnunuzi atafuata maziwa kwenye vituo vilivyopangwa kikiwamo Kituo cha Komaswa, Kata ya Manga ambacho kimeshaandaliwa kwa ajili ya uuzaji maziwa.

ALLIANCE GINNERIES LTD WASHAURI SERIKALI ITOE ELIMU UBORA WA MBEGU MPYA




UONGOZI wa kinu cha kuchambua zao la Pamba cha Alliance Ginneries Ltd, Wilayani Bariadi, Simiyu umeishauri Serikali itoe elimu kuhusu ubora wa mbegu mpya ya UKM08 ili kuondoa mkanganyiko kwa wakulima na kuiondoa sokoni mbegu ya UK91 ili kuimarisha na kuboresha kilimo cha mkataba.

Pia kampuni hiyo imewekeza kwa kusambaza tani 20,000 za mbegu hiyo aina ya UKM08 kwa wakulima wa mashamba darasa, katika vijiji vya Ikungulyabeshi, Nguliati, Kilalo, Ikungulyabashashi na Nyamagana, Kata ya Kasoli.

Ushauri huo ulitolewa juzi na meneja wa kinu hicho cha Alliance, Boaz Ogola, alipozungumza na waandishi wa habari, waliotembelea mashamba darasa yanayosimamiwa na kinu hicho mkoani Simiyu, baada ya kumalizika kwa mkutano wa wadau wa zao la pamba (Ginners) wa Wilaya za Bariadi na Itilima, kuhusiana na kilimo cha mkataba na changamoto zake.

 Alisema mbegu ya UK91 ambayo imedumu sokoni kwa kipindi cha miaka zaidi ya 10 imechoka, hivyo kusababisha wadudu waizoee na kuishambulia kwa urahisi, ambapo aliwataka wakulima kuacha kuitumia na kuendelea nayo ni kuzidi kujididiza kiuchumi.

Ogola alisema madai ya baadhi ya wakulima na wanasiasa kuwa mbegu hizo za UKM08 zisizo na manyoya hazioti ni uongo uliopitiliza, bali zimeonesha kuwa na tija kwa wakulima tofauti na mbegu ya UK91 ambayo uzalishaji wake kwa ekari ni kilo 200 hadi 300.

"Kitaalamu ili pamba iwe na tija kwa mkulima, mbegu isikae sokoni kwa miaka 10, inachoka na wadudu wanaizoea, hivyo nguvu ya uzalishaji inapungua. UK 91 imechoka sasa inapaswa iondoke badala yake wakulima watumie UKM08 ambayo imeonyesha tija na ina uwezo wa kuzalisha kilo 800 hadi 1,200 kwa ekari,"alisema Ogola na kuongeza;

"Uwekezaji huo wa tani 20,000 za mbegu za UKM08 kwa wakulima tulioingia nao mkataba, tunaamini baada ya miaka miwili tani milioni 1,440,000 zitakuwa zimezalishwa mbegu za kutosheleza mahitaji ya wakulima," alisema.

Alisema mbegu hizo zina tija kwa pande zote kwa mkulima na mchambuaji endapo zitapandwa na kutunzwa kitaalamu na baada ya kuvuna na kuchambuliwa pamba hiyo mbegu bora zitapatikana kwa asilimia 75. 

 

 Alidai kwamba baada ya kuchambuliwa kwa pamba uzalishaji wa nyuzi ni asilimia 33, mbegu asilimia 63 na asilimia 2 ni taka (west) kulinganisha na mbegu ya UK91. Hivyo serikali haina budi kuiondoa mbegu ya UK91 sokoni ili wakulima watumie UKMO8 ambayo ina tija kwao na yenye uwezo wa kuzalisha kilo 800 hadi 1,200 kwa ekari.

Aidha mratibu wa Mpango wa Kuendeleza Kilimo cha zao la Pamba na Viwanda vya nyuzi (CDTP), Donald Sayi, aliwataka wawekezaji wa zao hilo kutokana na uzalishaji wake kushuka waangalie na kuwekeza kwenye maeneo wanayoweza kupata faida.

Alisema wakulima wanawategemea wawekezaji hao ambao ni wanunuzi na wachambuzi, hivyo mapato yao yakiimarika, halmashauri pia zitapata mapato mazuri na kuzishauri zitenge asilimia 10 ya mapato hayo kwa ajili ya elimu ya huduma za ugani kwa wakulima.
"CDTP hatuna nia ya kumweka mtu pembeni, tunataka twende sote kwani mafanikio ni yetu wote. Wakulima wapate faida kwa jasho lao kadhalika na wachambuzi pia. Kipato kikiimarika kati ya wakulima na wachambuzi ni faraja kwetu,"alisema Sayi.

Alisema kilimo cha mkataba cha zao la pamba kinafadhiliwa na Tanzania Gatsby Trust (TGT), ambapo CDTP ni washauri, lakini baadhi ya wanasiasa wamekuwa wakikipinga kwa madai kuwa wanunuzi na wachambuaji wa zao hilo wanawanyonya wakulima kwa kuwakopesha pembejeo, mbegu na viuadudu, jambo ambalo si kweli.


Thursday, March 6, 2014

SERIKALI YATANGAZA TAREHE YA USAILI KWA WAOMBAJI WA NAFASI ZA KAZI ZA KILIMO NA MIFUGO








Serikali inapenda kuwaarifu waombaji wa nafasi za kazi kwa tangazo la tarehe 27 Novemba, 2013 wa kada za Kilimo, Mifugo, Uvuvi na Udereva kuwa usaili utaanza tarehe 4 Machi, 2014 takriban katika mikoa yote Tanzania Bara na Zanzibar.

Katibu wa Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma Bw. Xavier Daudi amesema hayo leo ofisini kwake wakati akiongea na baadhi ya wadau waliomtembelea kwa lengo la kufahamu masuala mbalimbali ya uendeshaji wa mchakato wa ajira serikalini.

Amesema usaili huo unaoanza tarehe 4 Machi katika mikoa takribani yote nchini utahusisha jumla ya wasailiwa 6,087 wa fani za Kilimo, Mifugo, Uvuvi na udereva kwa kada ambazo sio za Maofisa. Amefafanua kuwa vigezo vya kupanga mikoa ya usaili vimetokana na anwani ambazo waombaji waliwasilisha katika barua zao za maombi husika ya kazi.

Daudi alibainisha kuwa kila mwombaji aliyekidhi vigezo na kuchaguliwa kwa ajili ya usaili anapaswa kwenda kufanyia usaili katika mkoa aliopangiwa kama anwani yake inavyoonyesha katika tangazo kwenye tovuti ya Sekretarieti ya Ajira, isipokuwa kwa waombaji wa mkoa wa Katavi wao wataenda kufanyia usaili mkoa wa Rukwa na waombaji waliotumia anwani za mkoa wa Singida wao watafanyia usaili mkoa wa Manyara kutokana na sababu zisizozuilika.

Aliongeza kuwa kwa mwombaji ambae hatazingatia anwani, siku na muda aliopangiwa na kuamua kwenda mkoa mwingine tofauti na utaratibu uliopangwa ajue wazi hatasailiwa kwa kuwa ratiba na idadi ya majopo ilishapangwa kwa kila mkoa na haitabadilishwa ili kuweza kurahisisha kazi hiyo kukamilika  kwa ufanisi.

Aidha, amewataka waombaji wote wa tangazo hilo kutembelea tovuti ya Sekretarieti ya Ajira  ambayo ni http://www.ajira.go.tz/  wao wenyewe ili kuweza kujua kiundani endapo wamechaguliwa kufanya usaili, kufahamu tarehe, mahali na muda wa kuanza usaili ili kuepuka usumbufu usiokuwa na lazima.

Daudi aliendelea kufafanua kuwa kwa waombaji waliotumia anuani za mkoa wa Dar es Salaam kwa nafasi ambazo sio za maofisa usaili utafanyika tarehe 11 Machi, 2014.

 Aidha, kwa nafasi za Maofisa Kilimo, Mifugo na Uvuvi wote usaili wao utafanyika jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 10 hadi 14 Machi, 2014.
Katibu  amewataka waombaji wote kuhakikisha pindi wanapoenda kwenye usaili wawe wamejiandaa vya kutosha ikiwemo kubeba nyaraka muhimu hususani vyeti halisi vya taaluma zao maana vitahitajika kwa ajili ya uhakiki siku ya usaili. Aidha, amewasihi waombaji wa matangazo mengine ya nafasi za kazi kuwa na subira wakati uchambuzi ukiendelea na pindi utakapokamilika wahusika watataarifiwa.

Alimaliza kwa kuwasisitiza wadau wa Sekretarieti ya Ajira kuwa pindi wanapoona matangazo ya kazi, ikiwemo kuitwa kwenye usaili au kupangiwa vituo vya kazi katika vyombo mbalimbali vya habari hususani baadhi ya mitandao ya kijamii wajiridhishe kwanza kwa kuangalia taarifa hizo katika tovuti ya Sekretarieti ya Ajira, ili kuepuka taarifa zisizokuwa za kweli ambazo zimekuwa zikitolewa nyakati nyingine na baadhi ya watu wasio waaminifu kwa lengo la kupotosha Umma.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini.
Ofisi ya Rais-Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa  Umma. 21 Machi, 2014
Kwa maelezo zaidi; wasiliana na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini.