Saturday, May 4, 2013

MAELEZO YA MSINGI KUHUSU KILIMO CHA MIGOMBA

 
UTANGULIZI
Ndizi ni zao linalolimwa katika ukanda wa tropiki na hutumika kwa ajili ya kupikia na kama matunda. Vilevile ndizi huweza kutengenezea starch, chips, pombe (mbege), ama kukaushwa na kuuzwa kama matunda yaliyokaushwa. Wakati mwingine ndizi hutumika kutengenezea unga ambao huweza kutumika kwenye supu, mikate, ugali na uji. Maua ya ndizi huweza kutumika kama mboga, ila ni lazima yachemshwe kwenye mji ya chumvi ili Kuondoa ladha ya uchungu. Majani ya mmea huu ni chakula kizuri cha kuku na wanyama na huwa na virutubisho aina ya protein kwa wanyama hawa. Pia majani haya hutumika kwa ajili ya kupakia vitu mbalimbali na kwa ajili ya kuezekea nyumba. Pia ni mazuri sana kwa kutandazia shamba ama bustani. Halikadhalika migomba hutumika kuzuiya ama kupunguza kasi ya upepo.


MAHITAJI YA MAJI, HALI YA HEWA NA UDONGO
Wakulima wa mwanzo kabisa wa ndizi walitokea huko Maleshia na kusini mashariki mwa bara la Asia. Huko ndizi ilikuwa ikilimwa kwenye udongo wenye rutuba nyingi sana na udongo wa volkano. Pia kwenye delta za mito na kandokando ama ndani ya misitu ambako udongo huwa na rutuba sana.
Ndizi hukua vizuri sehemu zenye joto kidogo na unyevu nyevu na mwinuko wa 0-1800 m kutoka usawa wa bahari . Aina nyingine kama ‘DWARF CAVENDISH’ huweza kusitawi hadi kwenye mwinuko wa mita 2100 kutoka usawa wa bahari (sehemu za milimani sana).
Mahitaji ya mvua ni ya wastani wa 1000mm kwa mwaka japokuwa migomba husitawi vizuri kama ikipata maji ya kutosha. Hii ni pamoja na kumwagilia kipindi cha kiangazi bila kutuamisha maji.
Halijoto ya 27°C hadi 38°C ndio ifaayo kwa kilimo cha ndizi na migomba hudumaa kama kuna baridi sana (chini ya 13°C.)
Upepo mwingi ni tatizo kwa migomba kwa kuchana majani na kuyaharibu pia kuangusha migomba. Kupanda migomba kwa vikundi husaidia kuzuiya upepo na ikibidi migomba iliyobeba ndizi iwekewe nguzo kama zinapatikana.
Udongo mzuri kwa kilmo cha ndizi ni tifutifu yenye uwezo wa kupitisha maji na hewa kwa urahisi. Udongo wenye mbolea nyingi ni mzuri sana kwa migomba.


UPANDAJI
Ndizi hupandwa kwa kutumia vichipukizi ama migomba midogo ama sehemu za viazi zenye uwezo wa kutoa vichipukizi. Uzao wa ndizi hutegemea sana aina na umri wa vichipukizi vilivyotumika wakati wa upandaji. Vichipukizi vizuri ni vile vilivyochongoka vyenye urefu wa sentimeta 75 na upana wa chini ya shina wa sentimeta 15 na majani yake yamechongoka. Hivi huzaa baada ya miezi 18 tangu hayajapandikizwa. Vipandikizi hutoa ndizi hata baada ya miaka 2-3. Migomba mikubwa wastani huzaa bada ya miezi 5-8. Vichipukizi maji vyenye majani mapana havifai kwa kupandikiza kwani huzaa ndizi ndogo na uwezekano wa kupona baada ya kupandikizwa ni mdogo.
VIPIMO
Miche ama vichipukizi vya migomba vipandwe kwenye shimo lenye urefu wa sm 60 na upana wa sm 60. Udongo uchanganywe vizuri na mbolea ya kutosha. Kama mvua hazitoshi, shimo liwe na urefu wa sm 150 na upana wa sm 100.
NAFASI
Kwa aina za migomba midogo nafasi kutoka mmea hadi mmea iwe mita 3, na kutoka mstari hadi mstari iwe mita 3. Migomba 1000 kwa ekari.
Kwa aina ndefu. Mmea hadi mmea mita 3 na mstari hadi mstari mita 4. Migomba 480 kwa ekari.
MUDA WA KUPANDA MIGOMBA
Muda muafaka ni mwisho wa msimu wa kiangazi ama mwanzo wa msimu wa mvua.
MCHANGANYO WA MAZAO
Mazao kama kahawa, mahindi,mbogamboga, papai, miti ya matunda, kivuli na mbao, na mikunde kunde.
MATUNZO
Wiki 4-6 tangu migomba ipadwe, inapaswa kupaliliwa. Pia migomba inafaa kupangiliwa kwa mafungu. Migomba isizidi minne kwa kila kifungu. ‘KISUMU’, vichipukizi vyote viondolewe kubaki na mgomba mmoja mkubwa, na midogo mitatu yenye umri tofauti tofauti ili kupata mazao mwaka mzima.
Migomba mingi sana husababisha kuzaa ndizi ndogo. Vichipukizi vyenye afya ndio vibakishwe, Uchaguzi ufanyike kufuata nafasi iliyopo. Vichipukizi visivyotakiwa vikatwe na kuharibiwa sehemu inyokua.
KUTANDAZIA
Matandazo ni muhimu sana na ikibidi yawekwe shamba zima. Matandazo yawekwe umbali wa sm 60 kutoka kwenye kila fungu la migomba. Hii inasaidia Kuepuka wadudu waharibifu kwenye mizizi ya migomba.
MBOLEA
Migomba huhitaji sana mbolea ili izae vizuri. Mimea aina ya mikunde kunde inaongeza rutuba kwenye udongo kama ikipandwa shambani. Pia mbolea ya samadi na mboji ni muhimu sana. Kama kipato kinaruhusu tunashauriwa kutumia mbolea ya miamba ya Minjingu; ‘MINJINGU ROCK PHOSPHATE’ kwa ajili ya kuboresha na kuimarisha mizizi ya migomba.
MAGONJWA NA WADUDU WANAOSHAMBULIA MIGOMBA
Bacterial wilt(Mnyauko wa bacteria).
Mwanzoni jani mojawapokati ya majani machanga matatu huanza kuwa njano na kuvunjika. Baadae majani mengine hunyauka na kudondoka kuzunguka shina la mgomba. Ndizi iliyoshambuliwa na ugonjwa huu huwa na madoadoa kwa ndani kama inavyoonekana.

 

NINI CHA KUFANYA
 Tumia aina zinazostahimili ugonjwa huu kama zipo.
 Tumia vichipukizi visivyo na ugonjwa huu.
 Ondoa migomba yote iliyoathirika na uiteketeze.
UGONJWA YA VIRUSI
BUNCHY TOP

Ugonjwa huu huweza kutokea wakati wowote wa ukuaji wa migomba.
Huenezwa na aphids na hushambulia hata vichipukizi. Mimea iliyoathiriwa huweza kushindwa kuzaa na ama ikizaa huzaa ndizi ndogo na ngumu.
NINI CHA KUFANYA
 Tumia vichipukizi visivyo na ugonjwa huu.
 Ondoa kabisa migomba yenye dalili za ugonjwa huu, pamoja na viazi vyake na teketeza.
 Thibiti aphids ambao ndio waenezaji.
MAGOJWA YA FANGASI
MICHIRIZI MEUSI (Black leaf streak )
Ni ugonjwa hatari sana wa migomba na unashambulia majani ya ndizi. Vimelea vya ugonjwa huu husambazwa na upepo na hukua vizuri kwenye hali ya unyevunyevu. Sehemu za pembezoni mwa jani huanza kukauka na hatimaye jani zima hufa.
Ugonjwa huu husababisha mazao duni na ndizi kuiva kabla ya kukomaa.


 
NINI CHA KUFANYA
 Ondoa na haribu kwa moto majani yaliyoathirika. Vinginevyo ondoa majani yaliyoathirika na weka mbali na shamba la migomba ama fukia chini sana.
 Epuka kumwagilia majani kwa juu, tunashauriwa kumwaga maji kwenye shina.
Epuka kupanda kwenye msongamano.
UGONJWA WA PANAMA (Fusarium wilt).
Huu ni ugojwa utokanao na fangasi waishio ardhini na hushambulia mizizi na kuziba njia za kusafirisha maji na madini kwenye mmea, kwahiyo mmea hunyauka na kufa. Majani huwa ya njano na hatimaye kukauka
NINI CHA KUFANYA
 Tumia migomba inayostahimili huu ugonjwa kama Dwarf Cavendish.
 Kusafisha shamba na Kuondoa visiki vilivyo shambani huweza kusaidia kupunguza ugonjwa huu.
 Majivu yanaweza kuwekwa kuzunguka
(UGONJWA WA MUOZO SIGARA) THE CIGAR END ROT DISEASE
Ugojwa huu unaweza kuathiri matunda ya ndizi yaliyoiva, na kusababisha kuoza na kukauka kwa ndizi kuanzia mwisho. Palipoathirika huwa na ungaunga kama majivu.Huonekana kama sigara iliyozimwa. Ugojwa huweza kuendelea hadi wakati wa kuhifadhi ama kusafirisha. Huweza kuharibu mkungu mzima na kusababisha hasara kubwa.
NINI CHA KUFANYA
 Zingatia usafi shambani.
 Epuka kujeruhi ndizi na usikate ua la ndizi wiki 8-11 tangu izae.
ANTHRAC NOSE
Huu ni ugonjwa unaoshambulia ndizi baada ya kuvuna, hasahasa wakati wa kuhifadhi na kusafirisha. Madoa madogo ya kahawia ama jeusi huanza kutokea kwenye ndizi. Mara nyingi hushanbulia ndizi zilizokomaa vizuri. Hushamiri vizuri kukiwa na hali ya unyevunyevu
Anthracnose Anthracnose fruit rot on banana


NINI CHA KUFANYA
 Hakikisha usafi shambani
 Punguza kujeruhi ndizi.
 Ziweke ndizi kwenye maji ya moto 50° kwa dakika 5.
 Kunyuzia mafuta ya jatrofa yaliyochanganywa na maji huzuiya anthracnose hadi siku 12

Thursday, May 2, 2013

Kikwete kufungua kongamano la kikanda la kilimo

RAIS Jakaya Kikwete anatarajiwa kufungua kongamano kubwa la kikanda la kilimo la muungano wa umoja wa vyama vya kilimo Kusini mwa Afrika (SACAU), lililopangwa kufanyika kuanzia Mei 13 hadi 15 mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Kongamano hilo litakaloangalia kwa undani suala la jinsi ya kuhudumia kifedha kilimo cha Afrika linatayarishwa na Baraza la Kilimo na Mifugo Tanzania (ACT) kwa kushirikiana na SACAU.
Akitangaza kongamano hilo jijini Dar es Salaam jana, Ofisa Mtendaji Mkuu wa SACAU, Ishmael Sunga, alisema litashirikisha washiriki zaidi ya 200 kutoka nchi 14 za Kusini mwa Afrika pamoja na wawakilishi wa vyama vya wakulima kutoka maeneo mengine ya Afrika. Sunga alisema pamoja na mambo mengine, mkutano huo utaangalia ushirikiano kati ya SADC/COMESA/EAC katika masuala ya kilimo.
“Mkutano utaangalia ushirika huo kwa undani, muundo wake na umuhimu wake kwa wakulima na biashara katika sekta hii ya kilimo,” alisema.
Pia mkutano huo utaangalia makisio ya mahitaji ya bidhaa za kilimo duniani na kuona fursa na tishio lake kwa wakulima.
Kwa mujibu wa Sunga, kongamano hilo litaangalia kama mfumo wa kifedha uliopo sasa unaweza au hauwezi kuendeleza sekta ya kilimo katika siku zijazo.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa ACT, Janet Bitegeko, alisema kongamano hilo litakalokusanya wakulima toka sehemu mbalimbali Afrika litashuhudia kuzinduliwa kwa mradi wa majaribio wa kilimo wa SACAU nchini.
Alisema kuwa inatarajiwa kongamano hilo litakuja na majibu thabiti ya jinsi ya kuinua kilimo nchini, katika kanda na Afrika kwa ujumla.
ACT ni chama kinachounganisha wadau mbalimbali wa kilimo hapa nchini.

Wazalishaji kilimo hai kupata soko la kimataifa

WAZALISHAJI wa mazao ya chakula yanayozalishwa kwa mfumo wa kilimo hai nchini wana fursa ya kuuza mazao yao kwenye soko la kimataifa ikiwa watazingatia viwango vya kimataifa vya usalama wa chakula na kuzingatia taratibu bora za kilimo.
Hayo yalielezwa jijini Dar es Salaam juzi na Mratibu wa Mtandao wa Trade Africa Network Tanzania, Deusdedit Kizito, alipozungumza na waaandishi wa habari kuelezea ziara ya mafunzo ya wiki mbili nchini Ujerumani katika maonesho ya biashara ya Fruit Logistica ya Berlin na maonesho ya bidhaa za kilimo hai ya BioFach, Nuremberg, Ujerumani.
Kizito ambaye pia alikuwa kiongozi wa msafara huo alisema ziara hiyo imefungua milango kwa wazalishaji wa bidhaa zinazotokana na kuzalishwa kwa mfumo wa kilimo hai nchini, kwani wanaweza kuomba na kupatiwa mikopo ya kuendeleza biashara zao kutoka kwenye mashirika ya kimataifa ambayo yameonesha nia ya kukuza biashara hiyo nchini iwapo watakuwa wamepata wanunuzi wa bidhaa zao Ulaya.
“Mikopo hiyo itatumika kukuza mitaji yao kwa kujenga mahala pa kuhifadhia bidhaa zinazozalishwa ikiwamo vyumba vya baridi, magari yenye majokofu kwa ajili ya usafirishaji wa matunda na mbogamboga na pia gharama za kuuza bidhaa nje ya nchi,” alisema.
Aliongeza kuwa mashirika hayo yanaweza kutoa mikopo hadi asilimia 80 ya thamani ya biashara husika na kuongeza kuwa yanatoa mikopo kwa miradi ya maendeleo kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati (SME’s), vyama vya ushirika kwa kugharamia mtaji wa uendeshaji na shughuli nyinginezo.
Pia alisema ziara hiyo imefanikisha upatikanaji wa masoko ya bidhaa za asali, kahawa, viungo vya aina mbalimbali, matunda halisi na yaliyokaushwa hasa maembe, nanasi, maparachichi na pensheni.
Kutokana na ziara hiyo, mtandao huo unaishauri serikali kuwa na sera za wazi kuhusu matumizi ya ardhi kuhusiana na wakulima wanaolima kwa kuzingatia mfumo wa kilimo hai na uhifadhi wa ardhi na wakulima wengine wasiozingatia mfumo huo.
“Pia serikali inapaswa kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Trade Africa Network Tanzania kama inavyofanya kwa Sido na Tan Trade. Hii inatokana na ukweli kuwa Trade Africa Network Tanzania inalenga kuendeleza ubora na kuongeza thamani ya bidhaa za wazalishaji wadogo ili waweze kukuza kwenye soko la kimataifa,” alisema.
Wakati huohuo, Kizito alisema maadhimisho ya Siku ya Uhuru wa Afrika mwaka huu yatafanyika kuanzia Mei 23 na kilele kuwa Mei 25. Maadhimisho hayo yatafanyika katika viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam.

Monday, April 29, 2013

Wizara Kufufua Mifumo Asili ya Kilimo



Mfumo wa Kilimo cha asili aina ya Kiamba unaotumiwa na kabila la Wachaga.

Wizara ya Kilimo Chakula na Ushirika imeanzisha Mradi wa kufufua Mifumo muhimu ya asili ya kilimo Duniani (Global Importance Agricutural Heritage System- GIAHS) ili kuendeleza Kilimo cha asili (Oranic Farming) na kumpunguzia mkulima gharama za uzalishaji.
Mradi huo unatekelezwa na Shirika la chakula Duniani (FAO) ambao unalenga kutambua mifumo ya asili na endelevu ya kilimo na ufugaji ili kumsaidia mkulima.
Afisa Mkuu wa Kilimo kutoka Idara ya Matumizi Bora ya Ardhi Bw.  Firmat Banzi
alisema mradi unagharimu zaidi ya dola laki mbili ambazo zimetolewa na Serikali ya Ujerumani.

Alisema kuwa katika Afrika Mashariki nchi ya Tanzania na Kenya ilichaguliwa kufufua mifumo hiyo kwa kuwa na sehemu muhimu za kilimo zanazotumia mifumo hiyo.
Aliongeza kuwa baada ya kuchaguliwa nchi ya Tanzania ilipendekeza mifumo mitatu ya kilimo asili ambayo ni Kihamba ambao hutumiwa na wachaga, Ndiva wa Wapare na Ngoro ambao hutumiwa na kabila la wamatengo.
Alifafanua kuwa mifumo hiyo mitatu ilifanyiwa utafiti na baadaye mfumo wa kichaga ulichaguliwa na kuanza kutumika. 
Aidha, alisema kijiji cha Chimbe juu kilichopo wilaya ya Moshi mkoani Kilimanjaro ndio kilichonufaika na mradi huo na sasa unafikia hatua ya mwisho katika utekelezaji wake.
Hatua hiyo imekuja baada ya tafiti mbalimbali kuonesha kushuka kwa bei ya zao la kahawa na kusema kuwa kilimo asili huongeza bei za mazao kwa kuwa mazao yanayolimwa hayatumii kemikali na badala yake hutumia mbolea ya asili kama vile samadi, aliongeza Bw. Banzi.
Mradi huo utasaidia kuboresha zao la kahawa kwa kutumia mbinu husishi za  kukabiliana na wadudu waharibifu wa mazao.
Alifafanua kuwa  mradi unajumuisha utayarishaji wa vitalu vya miche, ukarabati wa mifumo asili ya umwagiliaji na utayarishaji wa mbolea za asili kama vile samadi.
Ili kuhakikisha mradi huu unaendelea Bw. Banzi alisema wameshirikisha wadau mbalimbali ambao watasaidia kuangalia kwa karibu maendeleo ya mradi, alitaja wadau hao kuwa ni Chama cha Ushirika KNCU cha Kilimanjaro pamoja na halmashauri ya wilaya.
Mifumo ya asili ya kilimo ilianza kupendekezwa dunia toka mwaka 2002 na baadhi ya nchi zimeanza kutumia mifumo hii, baadhi ya nchi hizo ni Japani, Philipino, China na Ujerumani.

Chamwino walia njaa

KUTOKANA na ukosefu wa mvua ya kutosha katika Wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma, wakazi wake kwa sasa wanakabiliwa na baa la njaa, hali inayosababisha baadhi yao kukimbia familia zao.
Hayo yalielezwa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya wilaya hiyo, Laurent Hoya, wakati alipokuwa akifungua kikao cha baraza la madiwani.
Hoya alisema kuwa hali ya chakula katika maeneo mengi wilayani humo ni mbaya kiasi ambacho wakazi wengi wanahitaji kupata chakula cha msaada haraka iwezekanavyo.
Alisema kutokana na mvua kutonyesha kwa kiwango cha kutosha ndiyo sababu ya wananchi kukosa chakula kutokana na mazao mengi kukauka kwa jua.
“Hata wale tuliowahamasisha walime mtama ambao ndio kama zao mbadala linalostahimili ukame lakini hakuna walichoambulia,” alisema.
Alisema kuwa viongozi wa halmashauri hiyo kuanzia ngazi za vitongoji wanatakiwa kufanya jitihada za haraka katika kuangalia ni namna gani wanaweza kutoa msaada.
“Nawaombeni tutoke na kauli moja hapa, hali ya chakula katika halmashauri yetu ni mbaya sana, mimi nimefanya ziara katika maeneo mengi nimejionea hali ilivyo, inatisha, chakula hakuna kabisa,” alisema.
Naye Ofisa Kilimo wa wilaya hiyo, Godfrey Mnyamale, alithibitisha kuwepo kwa uhaba mkubwa wa chakula, hali ambayo inatishia maisha ya wakazi katika maeneo mengi.
Mnyamale alisema kuwa kutokana na hali hiyo wabunge pamoja na viongozi mbalimbali wilayani hapo wamefanya ziara katika vijiji vyote 77 na kuwataka wananchi kutumia vizuri akiba ya chakula waliyo nayo.
Hata hivyo alitoa wito kwa wanachi wenye mifigo kuiuza ili waweze kununua chakula na kujiwekea akiba ya kutosha.

Friday, April 26, 2013

Ugonjwa hatari wa mahindi waingia nchini

Ugonjwa hatari unaoshambulia mahindi na kusababisha saratani kwa binadamu umeingia nchini na wakulima sasa wametahadharishwa kutokula mahindi hayo wala unga ambao haujakobolewa.
Mahindi yaliyoathiriwa na ugonjwa huo huota ‘fungus’ ambao ina sumu inayoitwa ‘Aflatoxin’ ambayo inaweza kusababisha madhara kwa wanyama na binadamu hususan ugonjwa wa saratani.
Mbali na kutikisa mikoa kadhaa na kusababisha hasara kubwa kwa wakulima, ugonjwa huo ambao umeanzia nchini Kenya unaendelea kusambaa kwa kasi na sasa umeingia pia nchini Uganda.
Awali ugonjwa huo uliripotiwa kuzikumba wilaya za Babati mkoani Manyara na Meatu mkoani Shinyanga tu, lakini sasa umesambaa hadi katika mikoa jirani ikiwamo Kilimanjaro.
Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro, Leonidas Gama jana aliithibitishia blog hii kuwa mkoa wake umekumbwa na ugonjwa huo na tayari umesambaa katika wilaya tatu; Moshi Vijijini, Siha na Hai. “Ni kweli baadhi ya wilaya zimekumbwa na ugonjwa huo, bahati mbaya sana hauna tiba na unasambaa kwa kasi... Wataalamu wanaendelea kuwaelimisha wakulima kutambua dalili zake,” alisema Gama.
Gama alisema endapo mkulima atabaini shamba lake kushambuliwa na ugonjwa huo katika hatua za awali, anachotakiwa kufanya ni kung’oa mimea yote ya mahindi na kuichoma moto.
Mkuu wa Wilaya ya Hai, Novatus Makunga alisema takriban hekari 14 zimeshambuliwa na ugonjwa huo katika shamba la Watawa wa Kanisa Katoliki Mailisita na shamba la mkulima wa Lambo.
Alisema tayari wataalamu kutoka Taasisi ya Utafiti wa Kilimo ya Selian (SARI) ya Jijini Arusha wamefika wilayani humo na kutoa tahadhari kwa wakulima juu ya athari za ugonjwa huo. Mfanyabiashara mashuhuri wa mjini Moshi, John Bennett anayemiliki mgahawa wa Golden Shower aliitaka Serikali kutoa elimu kwa wananchi na wafanyabiashara na kuchukua tahadhari.
“Utajuaje unga wa dona haukutokana na hayo mahindi au pumba ya chakula cha mifugo hayakutokana na hayo? Hili jambo ni zito sana si la kufanyia utani hata kidogo”alisema Bennett.
Mkulima wa Kijiji cha Kikavu Chini wilayani Hai, Justine Mvungi alisema wataalamu kutoka SARI wamewataka kuchoma moto miche ya mahindi ambayo watagundua imeshambuliwa.
“Wametuambia takriban shamba likishambuliwa, tung’oe mahindi hayo na kuyachoma moto, wametuambia kama tulishavuna basi tukoboe mahindi hayo maana kiini chake kina madhara,”alisema.
“Aliongeza kusema” hata tukikoboa mahindi tumeambiwa zile pumba zake tusiipe mifugo kwa sababu itaathirika… Ugonjwa huu wa mmea wa mahindi umeleta taharuki kubwa kwa wakulima na wananchi.”

Thursday, April 25, 2013

Waziri wa Kilimo atiwa msukosuko bungeni

 Hotuba ya Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Christopher Chiza imezidi kupingwa kwa madai kuwa imejaa majibu ya uongo kwa Watanzania.
Licha ya suala hilo, kitendo cha Waziri Chiza kupeleka mradi wa bwawa la umwagiliaji Wilaya ya Kakonko ambako ndiko jimboni kwake, kilionekana kuwakera wabunge.
Akichangia bajeti ya Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika juzi, Mbunge wa  Viti Maalumu, Azzah Hilali (CCM) alisema Hotuba ya Waziri Chiza ilitolewa bungeni bila ya kufanyiwa utafiti wa kutosha, kwani vitu vingi vinaonekana havina uhalisia.
“Mambo mengi hapa ya Waziri hayana ukweli, kwani unaposema chakula hutolewa kwa wananchi mara baada ya wakurugenzi kuleta maombi siyo kweli,” alisema Hilali.
Alisema tangu Oktoba mwaka jana, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, aliomba chakula cha msaada lakini kilipelekwa nusu Februari mwaka huu.
Pia, Mbunge huyo alikosoa hotuba hiyo kuwa imetumia jina la Waziri Mkuu vibaya, kwani kiongozi huyo aliagiza chakula cha msaada kupelekwa Shinyanga tangu muda mrefu, lakini hakuna kitu chochote kilichofanyika.
“Ndiyo maana tunasema mnadanganya, wewe fikiria hata hao wataalamu wenu mnaowatuma wanaishia maofisini, huku mnakuja kutoa taarifa kuwa wamefika huko na kufanya kazi, jamani Watanzania wamechoshwa kudanganywa,” alilalamika.
Kuhusu mradi wa bwawa la Kakonko, Mbunge huyo alimtuhumu moja kwa moja Waziri Chiza kuwa anapanga miradi ya maendeleo kwa upendeleo.
Alisema Serikali ilitangaza Kahama kuwa italisha Mkoa wa Shinyanga, lakini hakuna mradi hata mmoja ulioelekezwa wilayani humo, badala yake miradi imepelekwa maeneo yenye neema ya mvua na kuhoji dhambi waliyomfanyia Mungu.

Serikali yalaumiwa kupeleka mbolea ‘mbovu’ Nkasi

Mbunge wa Nkasi, Ali Keisy (CCM) ameilaumu Serikali kwa kutokuwa na mpango mzuri kwa wakulima wa Mkoa wa Rukwa, kwani imeshindwa kuwaondolea kero kubwa ya mbolea ya Minjingu ambayo ilipelekwa muda mrefu na kuonekana mbovu.
Keisy alisema Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ilipanga kuwasaidia wakulima wa ukanda huo mbolea ya ruzuku, lakini ilibainika mbolea yote tani 1,000 iliyopelekwa Mkoa wa Rukwa ilikuwa haifai.
“Hata hivyo, naishangaa Serikali yangu, hivi kweli huyo Minjingu ni nani na kwa nini ameiweka Serikali mfukoni kiasi hicho, mbona hamumshughulikii,” alihoji.
Alishangazwa na kitendo cha wizara hiyo kuendelea kuweka mbolea hiyo kwenye maghala kwa muda mrefu, huku wakisingizia kuwa watapeleka mbolea nyingi kuihuisha na kwamba, ni makosa kwani wangepaswa kukamatwa wakati huo baada ya kuifikisha.
Pia, Keisy alilaumu Serikali kwa kuendelea kuagiza mchele kutoka nje ya nchi, ilihali Tanzania kuna mchele mwingi wenye ubora ambao hauna soko.
Keisy alisema kama Serikali itakuwa makini kuwatengenezea miundombinu wakulima wa mpunga, haitapata tabu ya kuagiza mchele kutoka nje ya nchi.
Aliitaka Serikali iwe makini katika suala la kilimo nchini.

Monday, April 22, 2013

Wafugaji washauriwa Kutumia Simu za Mkononi

Arusha
 nchini wameshauriwa kutumia mfumo wa teknolojia wa simu za mikononi itakayosaidia kuboresha afya ya jamii kwa ujumla katika kuwasiliana na wataalamu pindi kunapotokea matatizo yakiwaemo magonjwa katika jamii zao.Hayo yalisemwa na Mtafiti wa Kuboresha na Ufuatiliaji wa Magonjwa kwa Njia ya Simu kutoka Taasisi ya Utafiti na Udhibiti wa Magonjwa Ambukizi Kusini mwa Bara la Afrika (SACDS), Profesa Ezron Karimuribo wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini hapa.
Alisema taasisi hiyo imekwisha wapatia elimu ya kutumia teknolojia hiyo mpya wafugaji pamoja na wataalamu wa afya na mifugo zaidi ya 30 kutoka Wilaya ya Ngorongoro.

Wakulima wa korosho wapata hasara ya Sh10 bilioni

 Wakulima wa zao la korosho mkoani Lindi wamepata hasara ya jumla ya Sh10 bilion kutokana na kuuza korosho kwa bei ya chini ya dira ya Sh1200.
Kufuatia hasara hiyo wakulima hao wameitaka Serikali iwafidie wakulima hao wa korosho kama ilivyo kwa wakulima wengine ambao huwa wanapata hasara nchini.
Hayo yalibainishwa mkoani hapa na Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Nachingwea, Abdallah Chikawe ambaye pia ni Mwenyekiti wa Jumuiya ya Serikali za Mitaa wa Mkoa wa Lindi (ALAT), wakati akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma.
Chikawe alisema wakulima wa zao la korosho wa Mkoa wa Lindi hawana imani na Chama Kikuu cha Ushirika mkoani Lindi cha Ilulu pamoja na COASCO.
Hata hivyo walimtaka Mkuu wa Mkoa wa Lindi afunge akaunti zote za Chama cha Ushirika cha Ilulu cha mkoani Lindi hadi hapo ukaguzi utakapofanywa .