Friday, March 13, 2015

UGONJWA WA MATUPA KWENYE MAHINDI (SMUT).




    Ugonjwa huu hushambulia sehemu za uzazi za mahindi. Mashambulizi hufanywa na aina mbili za vimelea jamii ya uyoga (ukungu) vijulikanavyo kwa majina ya kitaalamu kama Sphacelotheca reliana  na Ustilago maydis. Vimelea hivyo husababisha magonjwa ya aina mbili ambayo dalili zake zinafanana.
    Mimea iliyoshambuliwa na ugonjwa huu ama haizai kabisa ama inazaa kiasi kidogo ukilinganisha na jinsi ambavyo ingeweza kuzaa kama isingekuwa imeshambuliwa. Kwa hiyo mashambulizi ya magonjwa haya husababisha hasara ya mavuno. Inakadiriwa kwamba hasara ya mavuno inawezakuwa kidogo tu ama asilimia kumi (10%) au hata zaidi ya kiwango hicho, lakini kupoteza ni kpoteza hata kama ni kiwango kidogo.
    Ugonjwa wa "matupa" unaosababishwa na kimelea kijulikanacho kama Ustilago maydis hufahamika kama "Common Smut" kwa kiingereza. Dalili zake huwa kuota kwa uvimbe katika sehemu za mmea zinazokua kama vile punje za mahindi, mbelewele na hata kwenye majani. Uvimbe huo ukikauka na kupasuka hutoa vumbi jeusi kama masizi ambayo ndiyo viini vya/mbegu ya huo ugonjwa. Dalili ya msingi ya ugonjwa huu kwenye mhindi ni kwamba inawezekana kuwa na baadhi ya punje zilizoshambuliwa na zingine ambazo hazina dalili katika gunzi moja. 
   Ugonjwa wa "smut" unaosababishwa na kimelea kijulikanacho kwa jina Sphacelotheca relianahufahamika kama "Head smut" kwa kiingereza. Kama ilivyo kwa ugonjwa wa "smut" ya kawaida, dalili za ugonjwa huu hujitokeza mara nyingi katika hindi lenyewe  na mbelewele na mara chache katika shina la mhindi. Tofauti na ugonjwa wa "smut" ya kawida, katika ugonjwa huu badala ya mhindi kuathiriwa baadhi ya punje, hindi zima hujaa vumbi jeusi ndani ambapo kwa nje ni kama mfuko mweupe ambao kabla ya kukauka hufana na uyoga. Vumbi hilo jeusi ndilo viini vya kimelea. Vivyo hivyo kwenye mbelewele. Wakati mwingine mmea ulioshambuliwa na ugonjwa huu hudumaa na hushindwa kuzaa. Dalili nyingine ya ugonjwa huu ni mhindi kuotesha vijani vidogo badala ya mbelewele.
                                            

    Dalili za ugonjwa wa "Head smut"
    UDHIBITI WA MAGONJWA YA"SMUT" 
1. Tumia mbegu bora ingawa mpaka sasa haipo mbegu maalumu yenye kustahimili ugonjwa huu. Kwa kutumia mbegu bora, mkulima utajihakikishia  mavuno bora.
2.  Daima hakikisha unalima kilimo cha kisasa kikijumuisha urutubishaji wa udongo. Epuka kuijeruhi mimea uwapo shambani. Mimea iliyo na majeraha hushambuliwa kwa urahisi na ugonjwa huu. Pia dhibiti wadudu waharibifu ambao pamoja na madhara  mengine wanayosababisha pia huijeruhi mimea na kwa hivyo kurahisisha maambukizo ya ugonjwa huu wa "smut".
3.  Kila inapowezekana tumia kilimo cha kubadilisha mazao. Katika kubadilisha mazao ni vema kutumia mzunguko wa mazao yasiyoshambuliwa na ugonjwa wa "smut" kama vile ngano, shayiri, njegere, viazi na maharagwe.
4.  Unapolima hakikisha masalia mabua yamefukiwa chini sana.
Nawatakia wakulima wote maandalizi mema ya msimu wa kilimo.

No comments:

Post a Comment